Wednesday

MCHAKATO WA LULU KUPATIWA DHAMANA

                                                                LULU.
                        

Siku chache baada ya kupunguziwa makali ya kesi ya kuhusishwa na kifo cha msanii mwenzake, Steven Charles Kanumba, staa aliyefanya vizuri kwenye tasnia ya filamu, Elizabeth Michael ‘Lulu’ameombewa dhamana baada ya hati maalum ya dharura kutinga Mahakama Kuu Tanzania, Jumatatu iliyopita.

Mmoja wa mawakili anayemtetea msanii huyo, Peter Kibatala alisema kuwa wamewasilisha hati hiyo ili kuomba dhamana kwa mteja wao huyo.

“Tunajua kuwa wafanyakazi wengi wa mahakama kuu huwa likizo kipindi hiki hadi Februari Mosi hadi mwakani, lakini kuna majaji sita ambao huwa wanakuwepo kwa dharura, wanaweza kutusikiliza na kutenda haki,” alisema.

Kibatala alisema kuwa wanaamini Lulu ana vigezo vyote vya kuweza kupewa dhamana na kumfanya awe anatokea nyumbani wakati wa kusikiliza kesi yake.

“Jukumu kubwa ni kupewa masharti na mahakama kuu na kuangalia kama tutaweza kuyamudu ili mtuhumiwa aweze kupewa haki yake ya msingi,” alisema Kibatala.

Mwandishi wetu alizungumza na mmoja wa makarani wa mahakama kuu ambaye alisema kuwa hajaiona hati hiyo ya kuomba dhamana ya Lulu lakini ikifika wakati wowote wataifanyia kazi.

Hivi karibuni Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu ya jijini Dar ilihamishia kesi hiyo mahakama kuu baada ya mwendesha mashitaka wa serikali kubadili mashitaka ya kuua na kuwa ya kuua bila ya kukusudia, hali ambayo imepunguza makali ya kesi iliyokuwa ikimkabali mtuhumiwa huyo.

Lulu anahusishwa na kifo cha Kanumba kilichotokea Aprili 7, mwaka huu nyumbani kwake Sinza Kijiweni jijini na kuzikwa makaburi ya Kinondoni Aprili 9, mwaka huu.  
     

No comments: